Saturday, May 23, 2015

Watu watano wamekamatwa na viungo vya albino wakiwa wanavitafuatia soko

Polisi wilayani Kahama mkoani Shinyanga, imewakamata watu watano wanaotuhumiwa kukutwa na viungo vya mtu mwenye ulemavu wa ngozi (albino), wakiwa katika harakati za kuviuza.

Akizungumza
na NIPASHE jana, Mkuu wa kituo cha polisi wilayani Kahama, Leonard Nyandahu, alisema watu hao walikamatwa saa 7 mchana jana katika nyumba ya kulala wageni iitwayo Maji Hoteli, iliyopo Phantom, kata ya Nyasubi, wilayani Kahama.

Aidha, Kamanda wa Polisi mkoa wa Shinyanga, Justus Kamugisha, aliwataja watuhumiwa hao kuwa ni Bahati Kirungu (56), ambaye ni mwalimu wa Shule ya Msingi Katungulu kata ya Wendele, Mhoja John (24), wa Isagehe-Nzega na Bilia Busanda (39), mkazi wa Mogwa Nzega.

Wengine ni Shija Makandi (60) wa Isagehe-Nzega, Regina Kashinje (40) wa Isagehe-Nzega na Aboubakary Ally (25) ambaye alikuwa msiri wa kutafuta wateja, mkazi wa Isagehe- Nzega.

Kamugisha alisema Mei 19, mwaka huu asubuhi, mkuu wa upelelezi wa kituo cha polisi Nzega, alipata taarifa za mtu akitafuta wateja wa kununua viungo vya albino, walipoweka mtego walishindwa kumkamata na kuhamishia biashara yake wilayani Kahama.

Aidha, alisema maafisa upepelezi mkoa wa Tabora kwa kushirikiana na wale wa Kahama, walifuatilia nyendo za watu hao na kuweka mtego wa kuwakamata watu hao uliofanikisha kuwanasa.

Alisema jeshi la polisi wilayani Kahama, linaendelea kuwashikilia watu hao kwa mahojiano zaidi ikiwa ni pamoja na kuubaini mtandao wao pamoja na kuchukuliwa hatua kali za kisheria.

Kamanda Kamugisha, alisema serikali na jeshi la polisi itaendelea kuwasaka wauaji wa walemavu wa ngozi na kuhakikisha suala hilo linamalizwa katika mkoa wa Shinyanga.

No comments:

Post a Comment