Thursday, April 23, 2015

Jinsi ya kupamba ndani ya nyumba kama unaishi na watoto wa umri mdogo


Kwa sababu tu una watoto wadogo nyumbani haimaanishi utashindwa kuiweka nyumba yako kwenye muonekano nadhifu na wa kuvutia. Nimeongea na mbunifu wa ndani Bi Aisha Omari ambapo atatujuza jinsi ya kupamba nyumba yako na wakati huohuo ukiwa na watoto wadogo ndani.
Karibu Aisha!

“Ukiwa unaishi na watoto wadogo kuna vitu vinaweza kukuvunja moyo kama vile unarudi na kukuta meza yako ya kioo imevunjwa,
kochi limemwagiwa tomato sosi na kwa ujumla nyumba nzima imevurugwa imebadilika”, anasema Aisha. Ndipo hata kabla ya kupumzika unaanza kusafisha na kupanga upya, kwenye makala hii utafurahia Aisha atakayotushirikisha.

Kila nyumba ina utambulisho wa muonekano wake wa ndani  tofauti na nyingine. Huenda upo kwenye kipindi cha mpito nyumbani kwako kutoka mtoto aliyekuwa hajaanza kukaa kwenda kwenye anayeanza kutambaa na kutembea hadi miaka mitatu; ni kwa namna gani mapambo yako ya ndani yataendana na kipindi hiki? Ni mabadiliko gani makubwa utayotakiwa kufanya kipindi hiki?

Wazazi wenye watoto wadogo huwa wananiuliza kama inawezekana kuwa na nyumba iliyopambwa vizuri na kuwa na watoto ndani wakati huohuo. Jibu ninalowapa ni NDIO! Njia zifuatazo zitakuwezesha kupamba nyumba yako na ikawa na muonekano wa kuvutia hata kama unaishi na watoto wa umri mdogo kabisa.

Sehemu kubwa ambayo watoto wanapenda kucheza na kuchafua kwa vyakula na vinywaji ni kwenye viti na makochi. Hata kama utajitahidi kuwazuia namna gani mwishoni hivyo vita mzazi hutaviweza, utashindwa tu, kwani utatoka na kurudi na kukuta wameshamwaga kitu kwenye makochi au zuliani. Suluhisho lake ni weka sofa zenye kitambaa kisichoonyesha uchafu na pia vitambaa hivyo viwe ni vya kuvulika kiasi kwamba unaweza kuviondoa na kufua.

Mtoto mdogo anapokuwa anajifunza kutembea na kukimbia huku na huko akiwa ndani ya nyumba ni hatari kuwa na meza ndogo ya kioo. Kipindi hiki unatakiwa kuwa na mkakati maalum kwenye mapambo yako ya ndani, kwa mfano usiweke meza ya kioo au yenye ncha kali, badala yake weka ya mbao ya duara na hata kama utapata zile zilizoshonewa vitambaa juu itakuwa salama zaidi. Meza ya kioo ina uwezekano mkubwa wa kuangushwa au kupigwa na kitu na mtoto na hatimaye kuvunjika na kumuumiza vile vile, ambapo usingependa mapambo yako yamuumize mtoto.

Pia, watoto wadogo wana nguvu nyingi na wanapenda kupeleleza vitu. Sasa hii haimaanishi kuwa mapambo yako madogomadogo ya kioo uyafungie. Yahamishe yaweke juu sehemu ambapo hawafikii. Tumia shelfu za juu kwa kuwekea mapambo ya kuvunjika na za chini weka yale ambayo hayana shida hata akitaka kuyashika kupeleleza na atakuwa huru kuchezea. Usiweke mapambo ya kuvunjia kwa mfano vesi ya maua ya kioo kwenye meza ya kahawa kwa ajili ya usalama wa mtoto.
Sanaa za ukutani ni moja kati ya njia nzuri zaidi za kuongeza rangi na michoro kwenye chumba.Ongeza mapambo kwenye zile sehemu ambazo watoto wako wadogo hawafilkii. Picha za ukutani zilizo juu watoto ambao hawajawa na uelewa hawawezi kuzifikia.

Watoto wanapenda kuvuta pazia na kujificha nyuma ya pazia. Kwa kufanya hivi wanaweza kuzing’oa na pia kuzichafua. Suluhisho lake ni kuwa ukiwa na watoto wadogo weka pazia fupi, zinazopita dirisha kidogo tu, usiweke zile za kuburuza hadi sakafuni kwa kuwa zitakuwa kishawishi kwao kuzichezea.

Ukiwa na watoto wadogo ndani zingatia rangi za kuta na zulia. Huenda unapenda rangi za mwanga lakini mimi Aisha nakushauri kuwa ukiwa na watoto wadogo weka rangi za kufifia hadi pale watoto watakapokua ndio unaweza kubadili. Kwa mfano ukuta wa rangi ya kijivu ni bora zaidi kwa watoto kuliko mweupe, hali kadhalika na zulia vilevile.

Tukiwa tunajiamini na mapambo ya nyumba zetu inatufanya tupende mahali tunapoishi. Tunakuwa huru zaidi na kufurahia maisha kwa kiwango kikubwa zaidi, anasema Aisha. Kwenye kazi yangu ya ubunifu wa ndani nimegundua kuwa watu wengi wanajua wanachopenda, lakini shida ni jinsi ya kugeuza picha iliyoko kichwa kuwa ya kweli ndani ya nyumba zao.

Usikose makala ijayo hapahapa jumamosi ijayo ili upate siri za kufanya makazi yako yaonekane nadhifu.

Makala hii imeandaliwa na Vivi, kwa maswali au maoni tembelea www.vivimachange.blogspot.com

No comments:

Post a Comment