Tuesday, April 28, 2015

Kiganja cha mtoto albino wa Sumbawanga kimepatikana Mbozi kwa fundi seremala....Mseremala huyo alimwagiza mpiga ramli amletee kiganja cha abino kwa dau la sh milioni 100

Mtoto Baraka Cosmas (6) mwenye ulemavu wa ngozi (albino) akiwa amelazwa katika hospital ya Rufaa jijini Mbeya baada ya kukatwa mkono siku za hivi karibuni.


Kiganja cha mtoto Baraka Cosmas (6) mwenye ulemavu wa ngozi (albino) kilichokatwa Machi 8 kwenye Kijiji cha Kipeta, Sumbawanga Vijijini kimepatikana mwishoni mwa wiki wilayani Mbozi.

Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mbeya,
Ahmed Msangi alisema juzi mjini hapa kwamba kiganja hicho kilipatikana kutoka kwa mkazi wa Kijiji cha Malonje, Sajenti Kalinga (54) ambaye anafanya kazi ya useremala.

Alisema awali, polisi walimkamata mganga wa kupiga ramli aliyemtaja kwa jina la Gunela Shinji wa Kijiji cha Kipeta kuwa ndiye aliyehusika kukata kiganja hicho.

Alisema baada ya kumbana mganga huyo alimtaja Kalinga kwamba ndiye aliyemtuma kuleta kiganja hicho cha mtu mwenye ulemavu wa ngozi (albino).

“Tulimbana mtuhumiwa akatueleza kuwa aliyemtuma kiganja hicho ni Sajenti Kalinga kwa dau la Sh100 milioni,” alisema Msangi.

Kamanda Msangi alisema mtuhumiwa Shinji aliwapeleka polisi hadi kwa mteja wake huyo na kufanikiwa kumkamata.

“Polisi walifika nyumbani kwa mtuhumiwa Kalinga na walipomhoji kwa kina, alikitoa kiganja hicho na kuwakabidhi.”

Alisema hadi juzi, watu sita walikuwa wanashikiliwa kwa tuhuma za kuhusika na tukio hilo wakiwamo waliokamatwa mwaka jana na wengine mwaka huu.

Wanaoshikiliwa ni baba wa mtoto huyo, Cosmas Lusambo, mganga wa jadi, Miambo Kameta; Shinji na Kalinga.

Mtoto Baraka Cosmas aliyekatwa kiganja hicho amelazwa katika Hospitali ya Rufaa Mbeya akiendelea na matibabu chini ya uangalizi wa mama yake Prisca Shaaban (28) ambaye sasa ana watoto watano, wanne kati yao wakiwa albino.

Mama huyo alisema amepata taarifa za kukamatwa kwa watuhumiwa hao na kwamba ingawa hajui masuala ya kisheria, anaamini Serikali itachukua hatua stahiki kwa watakaobainika kuhusika.

Msangi alisema watuhumiwa hao watafikishwa mahakamani mkoani Rukwa wakati wowote.

MWANANCHI

No comments:

Post a Comment