Monday, April 27, 2015

Supermarket inayomilikiwa na Wachina Dar inabagua Watanzania weusi....Mtu mweusi haruhusiwi kuingia kununua bidhaa


DUKA la jumla (Supermarket) lijulikanalo kwa jina la Huarang lililopo Dar es Salaam linalomilikiwa na raia wa China, limejiwekea mazingira ya kupiga vita Watanzania wenye ngozi nyeusi kuingia ndani na kununua bidhaa.

Duka hilo liko katika Mtaa wa Ursino, Mikocheni katika kitalu namba 56 na mwandishi wa habari hizi ni miongoni mwa waathirika wa ubaguzi ambao ni wa aina yake hapa nchini.

Gazeti hili lilikuwa limepata taarifa kutoka katika vyanzo vyake vya habari kuhusu duka hilo na juzi Jumatatu waandishi wa gazeti hili walikwenda wenyewe kujionea nini hasa kinafanyika katika eneo hilo.

Kwa nje, duka hilo halina dalili kwamba linafanya shughuli hizo kwani limezungukwa na nyumba inayoonekana kama makazi ya kawaida ya watu kuishi, lakini mtu anapoingia ndani ndiyo ataona duka hilo ambalo huuza vyakula na vinywaji baridi vinavyopenda kutumiwa na watu wenye asili ya China.

Hapo awali, mmoja wa watu waliowahi kukumbwa na kadhia hiyo ya ubaguzi alilieleza gazeti hili namna alivyozuiliwa kuingia ndani ya duka hilo kwa maelezo kwamba hairuhusiwi.

“Ili gari yako iruhusiwe kuingia ndani ya duka hilo ni lazima uwe umempakiza mtu mwenye asili ya China la sivyo hawaruhusu. Mimi niliambiwa tu na nilipokwenda kujaribu nilikataliwa kuingia kwa madai kuwa siruhusiwi,” alisema mmoja wa waathirika wa ubaguzi huo ambao hata hivyo hakutaka kutajwa jina lake.

Waandishi wawili wa Raia Mwema waliingia katika eneo hilo kwa kutumia gari la ofisi lenye nembo ya kampuni lakini walipofika getini waliombwa na mlinzi wa kampuni ya ulinzi ya KK Security kusubiri kwanza ili akaulize ndani endapo wanaruhusiwa kuingia.

Hata hivyo, kabla ya kuondoka kuingia ndani, mlinzi huyo aliuliza ni aina gani ya bidhaa inayohitaji kununuliwa na waandishi hao; ambao walisema kwamba wanachohitaji ni tambi za Kichina maarufu kwa jina la Noodles.

Mlinzi huyo, pengine kwa kuhofu kwamba wahusika ni waandishi wa habari, alitoa ruhusa kwa gari kuingia baada ya kuzungumza na ‘mabosi’ wake ambao walikuwa ni raia watatu wa Kichina; wawili wanawake na mmoja mwanaume aliyekuwa akipokea malipo.

Mara baada ya waandishi hao kuingia ndani ya duka hilo, mmoja wa Wachina hao alianza kuzungumza kwa kufoka, akionyesha kuudhiwa na kitendo cha kuwaona wageni wasiotakiwa kwenye eneo lake la kazi.

Mwanamama huyo alikuwa akifoka kwa kutumia lugha ya Kichina na wakati mwandishi wa habari hizi alipomhoji mwanaume yule ni kwa nini mwenzake anafoka mara tu baada ya waandishi kuingia, muuzaji yule hakujibu zaidi ya kukaa kimya.

Baada ya kumaliza ununuzi, waandishi wetu walikwenda kufanya malipo lakini kwa kuuliza kwanza kwa nini duka lile halitaki kuhudumia watu weusi.

“Sielewi Kiingereza sana. Mimi si Meneja hapa na mwenyewe yuko mbali. Siwezi kuzungumza kwa niaba ya wahusika lakini sijui kama tunakataza watu weusi wasiingie. Sisi sote ni ndugu kwa nini tufanye hivyo,” alisema mhudumu huyo wa kiume.

Juhudi za kutaka kuzungumza na yule aliyekuwa akifoka hazikufanikiwa kwa vile kwanza alikuwa hataki kuonana ana kwa ana, na alikuwa akiondoka kila alipokuwa akiona dalili ya kutaka kusogelewa na waandishi wetu.

Wahusika wote dukani walionekana kuwa na umri unaokadiriwa kuwa kati ya miaka 30 hadi 40.
Waandishi wetu waliondoka ndani ya duka hilo lakini wakati walipokuwa nje na kuchunguza aina ya wateja wanaoruhusiwa, ilibainika kuwa wageni wazungu na wenye asili ya Kichina walikuwa wakiruhusiwa kuingia pasipo kuulizwa maswali yoyote na walinzi.

Mmoja wa walinzi waliowahi kulinda duka hilo alilithibitishia gazeti hili kwamba imekuwa kawaida kwa wamiliki kuwawekea vikwazo watu weusi kwa sababu ambazo hazijawekwa wazi hadi sasa.

“ Sisi tunapewa maelekezo tu kwamba akija mtu mweusi aulizwe getini anafuata nini. Akisema mara nyingi tunamwambia hakuna. Mtu mweusi pekee anayeruhusiwa kuingia ndani ni yule ambaye kafuatana na Mchina.

Bila ya hivyo huingii kabisa,” alisema mlinzi huyo aliyewahi kulinda hapo.
Mlinzi huyo aliliambia gazeti hili kwamba huenda wamiliki wana wasiwasi kwamba watu weusi wanaweza kuwaibia lakini alipoulizwa na waandishi wetu kwa nini ni watu weusi pekee wanaoonekana kuwa na uwezekano wa kuiba kwenye duka hilo na si watu wa asili nyingine, mlinzi huyo wa zamani hakuwa na majibu.

Alipoulizwa kuhusu tabia hiyo ya wafanyabiashara hao wa duka la Huarang, Waziri wa Viwanda na Biashara, Dk. Abdallah Kigoda, alisema alikuwa jimboni kwake Handeni, mkoani Tanga akishughulikia masuala ya kifamilia na hakuwa katika wakati mzuri kuzungumzia masuala hayo.

Juhudi za gazeti hili kuzungumza na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu (Uwekezaji na Uwezeshaji), Christopher Chiza, kuhusu suala hili hazikufua dafu kwa vile ofisini kwake alielezwa kuwapo ziarani nje ya Dar es Salaam na simu hakujibu simu wala ujumbe mfupi wa simu aliotumiwa kuomba kuzungumza.

Watanzania na Wachina wamekuwa wakiishi pamoja hapa nchini pasipo matatizo, huku Wachina wakifahamika kuwapo Tanzania tangu mwaka 1891 wakati walipoletwa na utawala wa kikoloni wa Wajerumani.

Walikuja nchini kwa wingi zaidi mwishoni mwa miaka ya 1960 wakati wa mradi mkubwa wa ujenzi wa Reli ya Tanzania na Zambia (Tazara) lakini wamekuja wengi zaidi kwenye miaka ya karibuni, baada ya Tanzania kufungua milango ya kiuchumi.

Kwa mujibu wa ripoti ya Shirika la Habari la China la XINHUA ya mwaka 2012, Tanzania inakadiriwa kuwa na raia wa China zaidi ya 10,000.

RAIA MWEMA

No comments:

Post a Comment