Wednesday, April 29, 2015

Jeshi la Nigeria limewaokoa wasichana 200 na wamama 93 kutoka kambi ya Boko Haram....Ila sio wale wa mwaka jana wa "Bring Back Our Girls"

Jeshi la Nigeria limesema limewaokoa watoto wa kike mia mbili na akina mama tisini na tatu kutoka katika kambi ya Boko Haram iliyoko katika msitu wa Sambisa, kaskazini mashariki mwa nchi hiyo. 

Jeshi hilo limesema watoto hao waliokolewa si kati ya wale waliotekwa
mwaka mmoja uliopita na kundi la kiislamu katika eneo la Chibok.

Jeshi limeiambia BBC kwamba 
wanawake na watoto hao wa kike walikutwa katika kambi nne tofauti ambapo silaha pia zimekamatwa,Msemaji wa jeshi amesema waliwapata wasichana hao baada ya kuziharibu kambi hizo.

"Ni muda mfupi tu uliopita, wanajeshi wetu wameingia katika msitu wa Sambisa, kutokea upande wa Alafa, ambapo walikuta kambi nne zinazomilikiwa na wapiganaji na kuziharibu, hapo ndipo walipogundua kuwa kuna wasichana wapatao mia mbili na wanawake tisini na tatu."

Kwa sasa jeshi limezuiwa kutoa utambulisho wa wasichana hao. Hata hivyo, jeshi limethibitisha kwamba wasichana hao sio wale wanafunzi waliotekwa katika mji wa Chibok.


"Tuko katika mchakato wa kuwachunguza hawa wasichana ili tuweze kubaini utambulisho wao, lakini kitu kimoja nataka nikiweke wazi kwa umma, tunapotaja idadi ya wasichana mia mbili, tayari watu wanaanza kufikiria wasichana mia mbili wa Chibok waliotekwa mwaka jana, hawa sio wasichana wa Chibok, tutaendelea kuwajuza kadri muda unavyokwenda iwapo kutakuwa na taarifa zozote. "

No comments:

Post a Comment