Saturday, April 25, 2015

MWILI WA MWANAFUNZI ALIYECHAPWA WAZIKWA....MCHUNGAJI AITAKA SERIKALI IANGALIE NAMNA YA KUWAADHIBU WATOTO SHULENI

Mwili wa mwanafunzi wa kidato cha pili katika Shule ya Sekondari Matui wilayani Kiteto Mkoa wa Manyara, Noel Bichima aliyefariki dunia kwa madai ya kuchapwa viboko na mwalimu wake, umezikwa jana kwenye Kijiji cha Matui.

Akizungumza kabla ya mazishi, Mchungaji wa Kanisa la
Anglikana, Parishi ya Malamka, Julius Matakala aliwataka wananchi wakubaliane na hali iliyotokea na wawe tayari muda wote kwa kuwa ni marehemu watarajiwa.

“Tunaiomba Serikali iangalie namna ya walimu wanavyotoa adhabu, lazima wafuate vigezo, kifo hicho kimesababishwa na uzembe ila watu waendelee kumuabudu Mungu kila mmoja na imani yake kwa kuwa hatujui siku wala saa,” alisema.

Wananchi waliokuwapo msibani hapo, walisikitishwa na kitendo hicho cha mwanafunzi kuchapwa hadi kufariki dunia, wakisema huo ni ukatili.

Hata hivyo, walisema wameliridhishwa na Serikali kuwakamata walimu watatu wanaodaiwa kusababisha kifo hicho.

Mjomba wa marehemu, Michael Mtwite akizungumza wakati wa mazishi alisema wameshafanya uchunguzi kwenye Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Dodoma na wanasubiri majibu.

“Lakini hatuhitaji uchunguzi sana kwa sababu viboko ndiyo vimesababisha kifo chake, viongozi wa Kiteto waangalie adhabu zinazotolewa shuleni na ziwe na viwango ili tukio kama hili lisitokee tena,” alisema Mtite.

Mwanafunzi huyo alifariki dunia kwa madai ya kuchapwa viboko zaidi ya 12 na walimu watatu wa shule hiyo Aprili 20, saa nne asubuhi baada ya kufeli mtihani wa Kiswahili kwa kupata alama 40.

Mkuu wa Wilaya ya Kiteto, Kanali Samwel Nzoka alisema walimu watatu wanashikiliwa na polisi wakidaiwa kusababisha kifo hicho.

“Mwalimu Peter Bajuta anadaiwa kumchapa viboko vinane, mwalimu Joyce Makongoro na mwalimu Sheila Ngereza wote kwa pamoja wanadaiwa kumchapa viboko viwili kila mmoja,” alisema.

MWANANCHI

No comments:

Post a Comment