Thursday, April 30, 2015

Mbunge Badwel aachiwa huru kwa kesi ya kutoa na kupokea rushwa..

Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, jijini Dar es Salaam, imemwachia huru Mbunge wa Bahi, mkoani Dodoma, Omary Badwel, (pichani) baada ya upande wa Jamhuri kushindwa kuthibitisha mashitaka ya kuomba na kupokea rushwa.
Kadhalika, mahakama hiyo imemuonya mbunge huyo kuacha kufuatilia maslahi na maisha ya watu na mali zao katika jimbo lake badala yake ajishughulishe na siasa na kutekeleza majukumu yake kwa jamii.

Hukumu hiyo ilitolewa jana na Hakimu Mkazi Mkuu, Hellen Riwa na kusema mahakama baada ya kupitia ushahidi uliotolewa na upande wa Jamhuri imeona bila kuacha shaka mshtakiwa hana hatia, hivyo inamuachia huru.

“Mahakama hii imeona ushahidi uliotolewa na Jamhuri mshtakiwa huna hatia na kwamba inakuachia huru… inawezekana kweli uliomba na kupokea rushwa lakini kwa ushahidi uliotolewa hauna mashiko ya kisheria wa kuweza kukutia hatiani, “ alisema na kuongeza:
“Kwa kuwa ushahidi haujathibitisha mashitaka yaliyokuwa mbele ya mahakama hii na kama unaingilia maslahi, mali na maisha ya watu huko jimboni kwako uache endelea kufanya mambo yako ya kisiasa.”

Alisema kwa mujibu wa ushahidi wa mazungumzo yaliyorekodiwa na wakati wa tukio uliotolewa mahakamani, sauti ya mshtakiwa haikusikika akiomba wala kushawishi rushwa, lakini amesikika aliyekuwa Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya ya Mkuranga, mkoani Pwani, Sipora Liana.

Alisema pamoja na mambo mengine, mshtakiwa ana wadhifa mkubwa na kwamba siyo rahisi yeye na kamati yote kuomba rushwa yenye thamani ya Sh. milioni moja kwa kila mjumbe.

Katika kesi ya msingi, ilidaiwa kuwa  mshtakiwa akiwa kama Mbunge wa Jimbo hilo, Mjumbe LAAC na mtumishi wa umma, alitenda kosa hilo kati ya Mei 30 hadi Juni 2, mwaka 2012 jijini Dar es Salaam.

Ilidaiwa kuwa  kinyume cha Sheria ya Kupambana na Kuzuia Rushwa, Mbunge huyo alishawishi kutolewa kwa  rushwa ya Sh. milioni 8 kutoka kwa Liana ili awashawishi wajumbe wa kamati hiyo wakati wa kupitia ripoti ya bajeti ya halmashauri hiyo ya mwaka 2011/12.

Ilidaiwa katika shitaka la pili kuwa, Juni 2, mwaka 2012, katika Hotel ya Peacock, jijini Dar es Salaam, mshitakiwa alipokea rushwa ya Sh. milioni moja kutoka kwa Liana kwa ajili ya kuwashawishi wajumbe wa LAAC kupitisha ripoti ya bajeti ya halmashauri hiyo ya mwaka 2011/12 bila vikwazo.

Hata hivyo, Mbunge huyo alikana mashtaka dhidi yake  na alikuwa nje kwa dhamana.


CHANZO: NIPASHE

No comments:

Post a Comment