Monday, April 20, 2015

MCHUNGAJI ATANGAZA KUGOMBEA URAISI MWAKA HUU

MHADHIRI wa Chuo Kikuu cha Kumbukumbu ya Stephano Moshi (SMUCCO), Mchungaji Godfrey Malisa, ametangaza nia ya kugombea urais Oktoba mwaka huu kwa tikeki ya mgombea binafsi.

Mchungaji Malisa, alitangaza azma hiyo
huku Serikali ikiwa bado
haijaweka bayana kuwepo kwa mgombea binafsi kwa sababu Katiba Inayopendekezwa haijapitishwa.
Mwaka 2010, Malisa aligombea ubunge Jimbo la Moshi kwa tiketi ya
Chama cha Tanzania Labour (TLP).

Akizungumza na waandishi wa habari mjini hapa jana, Malisa alisema amefikia uamuzi huo baada ya kuamini atachaguliwa.

Alisema ameamua kuchukua uamuzi huo ili kurejesha heshima ya
taifa, kama ilivyokuwa imejengwa na na Hayati Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Nyerere.

Hata hivyo, alisema enzi za Mwalimu Nyerere lilikuwa na heshima
kubwa ndani na nje ya nchi ambapo tangu kuondoka madarakani hajaweza
kupatikana kiongozi wa kuvaa viatu vyake.

“Mimi nimeishi Marekani na China…taifa letu
lilikuwa linaheshimika, leo hii hata amani imeanza kutoweka kutokana na maujai ya watu wenye ulemavu wa ngozi, ujambazi na wizi wa fedha za umma,” alisema.

Katika hatua nyingine, Malisa alisema Tanzania haipaswi kuitwa
nchi masikini kwani ina rasilimali nyingi, lakini imekosa viongozi
wa kuzilinda na kuzitumia kuinua uchumi wa taifa.

Alipoulizwa endapo nafasi ya mgombea binafsi 
haitakuwepo katika
uchaguzi huo, alisema kama Katiba iliyopo haitafanyiwa marekebisho na
kuwapo nafasi ya mgombea binafsi, atatangaza uamuzi mwingine.

MTANZANIA

No comments:

Post a Comment