Monday, April 20, 2015

Lowassa Athibitisha Ubora wa Afya yake baada ya Kutembea Kilomita 5 Kupinga Mauaji ya Albino

WAZIRI Mkuu wa zamani, Edward Lowasa, jana alithibitisha kwa vitendo kuwa afya yake iko safi baada ya kutembea umbali wa kilomita tano kwa miguu kwenye matembezi ya kupinga mauaji ya albino nchini.

Kwa muda mrefu, Lowassa ambaye ni mmoja wa makada wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) wanaotajwa kuwania nafasi ya urais katika uchaguzi mkuu wa Oktoba mwaka huu, amekuwa akidaiwa kuwa na matatizo ya afya na kuwa hawezi kuhimili mikimiki ya kampeni na shughuli nyingine zinazohitaji nguvu.

Lakini matembezi ya jana yaliyoongozwa na Lowassa kuanzia Uwanja wa Taifa wilayani Temeke mpaka viwanja vya TCC Chan’gombe na kutumia dakika 25, yamedhihirisha vinginevyo.

Matembezi hayo yalianzia barabara ya Mandela, Kilwa kupitia Temeke Mwisho, Wiles, Temeke Hospitali, Chang’ombe Polisi, Kiwanda cha Bia cha Serengeti na kuhitimishiwa viwanja vya TCC.

Akizungumza baada ya kuhitimisha matembezi hayo yaliyoandaliwa na kikundi cha Temeke Family Sport Club, Lowassa alisema hakushiriki matembezi hayo kwa lengo la kufanya siasa bali ni kumuunga mkono Rais Jakaya Kikwete katika vita dhidi ya mauaji ya albino.

“Hapa sikuja kufanya siasa, nimekuja kumuunga mkono Rais Kikwete katika suala la kupambana na kupinga mauaji ya albino,” alisema Lowasa.

MTANZANIA

No comments:

Post a Comment